aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Tuesday, February 18, 2014

Kagame adaiwa kupandikiza Makachero Nchini Kuipeleleza Serikali….Mbunge Atajwa kuhusika..!

JEURI ya wazi inayoonekana kuwemo ndani ya taarifa ambazo zimekuwa zikichapishwa mara kwa mara na vyombo vya habari  vya  serikali ya Rais Paul Kagame wa Rwanda dhidi ya Rais Jakaya Kikwete na serikali yake, inaelezwa kujengwa na ushirika wake wa kiintelijensia  alioupandikiza ndani ya mfumo wa  serikali  na taasisi mbalimbali hapa nchini,MTANZANIA limedokezwa. Taarifa zilizolifikia gazeti la  MTANZANIA  kutoka kwa  watu waliokaribu na viongozi wa Rwanda na wale walioko kwenye taasisi mbalimbali za kiserikali hapa nchini,zinaeleza kuwa taarifa ambazo zimekuwa zikiripotiwa na vyombo vya habari vya serikali ya nchi hiyo, msingi wake unaweza kuwa  mtandao ambao serikali ya Kagame imeujenga hapa nchini.
Kwamba Rwanda, mbali na kufanikiwa kupenyeza watu wake kwenye mifumo  ya kitaasisi hapa nchini, pia imefanikiwa kujenga ushirika na watu wa kada mbalimbali wenye umaarufu,ushawishi na wanaoheshimika nchini, wakiwemo baadhi ya wasomi na wanasiasa.
 paul
Kuvuja kwa taarifa hizi, kumekuja wakati ambao  gazeti la serikali ya Rwanda,Rwanda Times na mtandao wa News of Rwanda, yakiripoti taarifa zinazoigusa  serikali ya Rais Kikwete, ikinukuu vyanzo vya kutoka hapa nchini, japo ukweli wa taarifa hizo ukiwa haujulikani,kutokana na Ikulu ya Dar-es-salaam kuzikanusha mara kwa mara.
                                                                           
Dhana  hii inapewa nguvu na taarifa mpya kabisa  zilizotufikia, ambazo zinadai kuwa katika kuendelea kuimarisha mtandao  wake,  Serikali ya Rwanda  imechangisha  fedha  kwaajili  ya  baadhi ya vyama vya  siasa hapa nchini ili kulinda maslahi yake.Taarifa hizo  zinamtaja  Waziri wa Miundombinu  wa  nchi hiyo,  Profesa Silas Lwakabamba, ambae  aliwahi kusoma na kuishi nchini  kuwa ndiye aliye endesha  harambee hiyo  ambayo inadaiwa ilimshirikisha Rais Kagame.
Habari  zaidi ambazo MTANZANIA  imezipata zinadai kuwa katika harambee hiyo, iliyohudhuriwa  na baadhi  ya  Mawaziri wa serikali ya Rwanda  pamoja na wafanyabiashara wakubwa nchini humo,Rais Kagame kwa upande wake alichangia  Dola 500,000.
Gazeti hili limedokezwa kuwa, lengo la harambee hiyo, ni kuhakikisha ushawishi wake unafanikiwa, hasa kwa watu  ambao wamekuwa wakiiunga mkono Rwanda, hususani wakati huu mgumu ambao  inakabiliwa na tuhuma za kuchochea mapigano katika eneo la Mashariki ya Congo, ambako Tanzania imepeleka  wanajeshi wake.
Katika mkakati huo,  walengwa ni vyama  vya upinzani, kutokana  na kuwa na uhusiano  wa shaka na  serikali iliyoko madarakani.
Tayari mara kadhaa  vyombo vya  habari  Rwanda, hususani vile vya serikali, vimekuwa vikitumia  kauli zinazotolewa na wapinzani  hapa nchini, kama hoja ya utetezi wake dhidi ya uhusiano mbaya na Ikulu ya  Dar-es-salaam.
Profesa Lwakabamba, ambaye anatajwa kuongoza zoezi la sasa, inaelezwa kuwa serikali ya Rwanda imeamua kumtumia kutokana na uelewa wake kuhusu Tanzania.
Kabla ya taarifa hizi, Lwakabamba aliwahi kuripotiwa na gazeti moja (si MTANZANIA)  kwamba ni waziri mwenye asili ya Tanzania aliyechaguliwa katika serikali ya Rwanda.
Inaelezwa kabla ya uteuzi huo, alikuwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Rwanda, lakini pia alisoma  Chuo Kikuu Dar-es-salaam (UDSM)  Kitivo cha Uhandisi, na mwaka 1981 alikuwa Mkuu wa kitivo cha Uhandisi, kazi aliyoifanya mpaka anaondoka nchini.
Profesa Lwakabamba, ambaye anaelezwa kuijua vyema Tanzania kutokana na kuishi muda mrefu, alipata elimu ya msingi Muleba, mkoani Kagera na baadaye  kujiunga na shule ya sekondari ya Ihungo.
Mwaka 1971 na 1975 alipata Shahada ya Uzamivu  katika Kitivo cha Uhandisi, baada ya kujiunga na Chuo cha Leeds, Uingereza kwaajili ya shahada ya fani hiyohiyo.
Msomi  huyo anaelezwa kwenda Rwanda mwaka 1997,baada ya kuombwa na Rais Kagame, ambaye alikwenda UDSM kuwaomba baadhi ya wahadhiri kwenda Kigali kufungua chuo kikuu  katika taifa lake, baada ya kumalizika vita vya wenyewe kwa wenyewe mwaka 1994.
Gazeti hili lilimtafuta Profesa Lwakabamba kwa njia ya mtandao ili kupata ufafanuzi  kuhusiana na harambee hiyo, lakini hakuweza kujibu maswali aliyoulizwa.
 Juhudi za kumtafuta Profesa Lwakabamba bado zinaendelea. Wakati hayo yakitokea,taarifa nyingine zilizolifikia gazeti hili zinaeleza kuwa katika mkakati huo,mbunge mmoja (jina tunalo), hivi karibuni  alisafiri kwenda Rwanda  akipitia Afrika Kusini.
Inaelezwa kuwa mbunge huyo alionana na  baadhi ya viongozi wa serikali ya nchi hiyo, ikiwa ni sehemu ya mpango wa Rais Kagame kuhakikisha anaimarisha mtandao wake hapa nchini.
Mbali na mbunge huyo,taarifa hizo zimewataja baadhi ya wanasiasa  wengine ambao kwa muda mrefu  wamekuwa wakifaidika na fedha za serikali ya Rais Kagame, kwa kujua ama pasipo kujua  kama lengo lake ni kuwaweka katika mtandao wake huo.
Chanzo: Mtanzania.

No comments:

Post a Comment