aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Friday, February 21, 2014

HIVI NDIVYO WAGANGA WA KIENYEJI WANAVYOFANYA KAZI NA WACHEZAJI YANGA, SIMBA..!!

SUALA la ushirikina katika soka limekuwa likizungumzwa kama hadithi za kufikirika, wako ambao wanasema mambo hayo hayatokei, lakini wako ambao wamekuwa wakithibitisha kuwa hali hiyo inatokea.
Suala la ushirikina linakuwa katika sehemu mbalimbali, mfano wachezaji kwenda kwa waganga wa kienyeji maarufu kama wataalamu na kufanya kitu fulani ili kuwadhoofisha wenzao au wachezaji wanaocheza nao katika kikosi kimoja.
Wako ambao wamekuwa wakifanya kila linalowezekana kuhakikisha wachezaji wenzao wanaumia, katika soka suala hilo ni maarufu kama ‘misumari’ wakiwa na maana kuwa anayeumizwa, basi anakuwa amepigwa misumari.
Uchunguzi wa Championi kwa takribani mwezi mmoja na ushee, limekuwa likizunguka sehemu mbalimbali kufanya uchunguzi, ishu kubwa ilikuwa ni kuzungumza na watu mbalimbali na kutaka kujua kuhusiana na suala la ushirikina.
Inaonekana pamoja na kuwa na mambo mengi, suala hilo limegawanyika kwenye mambo mengi lakini matatu ndiyo yanaonekana kuchukua nafasi. Kwanza ni kuroga ili kuhakikisha timu inashinda, lengo hapa ni kuidhoofisha timu moja ili nyingine ishinde.
Suala la pili ni mchezaji kuhakikisha mmoja anaumia na kushindwa kabisa kufanya vizuri ili kumpa nafasi yeye aendelee kufanya vizuri na la tatu, mchezaji ni kusafisha nyota yake na kuidhoofisha ya mwenzake na hapo yeye atang’ara na kufanikiwa huku yule mwingine akifeli.
Katika watu mbalimbali ambao walifanya mahojiano na Championi Ijumaa, wengi wakiwa kutoka katika klabu kubwa za Simba, Yanga, Azam FC, Mtibwa Sugar, Coastal Union, wamekiri kuwa kweli ushirikina hufanyika.
“Hauwezi kusema uache kufanya ushirikina, sisi tumekuwa tukifanya kwa lengo la kujilinda na kupambana na timu pinzani. Kama wenzetu wanafanya hivyo, sisi tukikaa kimya maana yake tunakubali kuumia,” anasema mdau mmoja kutoka moja ya klabu kubwa za Tanzania.
“Uongozi unatutambua, kumekuwa hadi na fungu letu na lengo ni zuri  tu, kuilinda timu yetu na kuisaidia kufanya vziuri, kamwe hatulengi kumuumiza mtu,” anasisitiza.
Rekodi ziko nyingi sana kuhusiana na masuala ya ushirikina, hadi wachezaji Waafrika wale maarufu wanaocheza Ulaya kama Didier DrogbaSamuel Eto’o na wengine wamekuwa wakihusishwa na kufanya hivyo.
Mwaka 2009, mwandishi wa makala haya, alishuhudia baadhi ya waganga wa kienyeji nchini Ivory Coast wakiishi maisha ya juu kutokana na mamilioni ya fedha wanayoingiza. Uchunguzi wake ulionyesha kuwa wana fedha nyingi kwa kuwa wamekuwa wakifanya kazi ya kusafisha nyota za wachezaji maarufu wa nchini hiyo wanaocheza Ulaya kama Yaya & Kolo Toure, Drogba, Didier Zokora, Aruna Dindane na wengine.
Hapa vipi kuhusiana na suala hilo, Championi likaanza kukata mbuga likisaka mganga wa kienyeji ambaye amewahi kuifanya kazi yake hiyo vizuri kwa lengo la kuwasaidia wachezaji kuosha nyota zao.
Uchunguzi ulionyesha mganga huyo kijana na maarufu anapatikana eneo moja la vitongoji vya Jiji la Dar es Salaam na kazi ya kutafuta namba yake ikafanyika kupitia ndugu yake. Baada ya makubaliano, siku ya kwenda ‘kumtibu’ mchezaji huyo ikapangwa.
Waandishi wawili wa makala haya, Saleh Ally akajitambulisha kama meneja anayeishi barani Ulaya na mchezaji, Sweetbert Lukonge ndiye mchezaji anayetaka kwenda kucheza Ulaya, alitaka nyota yake ing’are kuanzia hapa nchini, baadaye Ulaya.
Miadi ikatengwa na siku ilipowadia, Meneja (Saleh) ambaye lafudhi yake kidogo ina Kiswahili cha shida kutokana na kuishi Ulaya siku nyingi pamoja na mchezaji (Lukonge) walifika kwenye kitongoji hicho na kupokelewa. Moja kwa moja, wakafikishwa hadi nyumbani.
Gari walilazimika kulipaki barabarani, halafu wakaingia mitaa ya ndani (si mbali sana) ambako gari halifiki na kwenda nyumbani kwa mganga huyo kijana, mahiri ‘kuwaponya’ wachezaji ili waweze kufanya vizuri katika soka.
Baada ya kufika, mganga aliuliza shida yao, maelezo ya meneja yalilenga kumsaidia mchezaji huyo ili amfunike mchezaji mwingine ambaye alikuwa akimzuia kupata namba kwa kuwa huyo meneja anataka mchezaji wake ang’are.
Mganga aliwahakikishia kuwa kila kitu safi kabisa na ndani ya siku chache baada ya tiba ya siku hiyo. Mambo yangekuwa mazuri lakini kulikuwa na bidhaa za kununua siku hiyo ili kuanza tiba.
Vifaa vilivyotakiwa ni kuku wawili, weupe na weusi, kitambaa, kipande cha sanda ambacho kimefukuliwa baada ya mtu kuzikwa. Yai na vingine ambavyo tayari viliandaliwa na mganga huyo.
Ikatolewa Sh 20,000 kwa ajili ya kununuliwa kuku wawili na bei ya ‘matibabu’ hayo ilikuwa ni Sh 300,000 hadi 400,000 ingawa kulikuwa na makubaliano kwa vile mganga anaonyesha si mtu wa tamaa na anayetaka ‘kusaidia’ watu.
Makubaliano yanafikiwa, meneja na mchezaji wake wanalazimika kumsubiri mganga anayefunga safari kwenda kununua kuku, baada ya kurejea anaomba muda mchache kuandaa vifaa vyake kabla ya kuanza kazi.
Baada ya hapo, mtoto mdogo anatumwa kuwaita wahusika (meneja, mchezaji) ambao baada ya kuingia kwenye chumba ambacho hufanyika kazi za mganga wanaelezwa kazi itakavyofanyika chumbani humo na baada ya hapo ni safari ya kwenda makaburini ili kuimaliza kazi hiyo huko.
Kidogo wawili wanaingiwa hofu, lakini mganga anawasisitiza hawapaswi kuwa waoga hata kidogo kwa kuwa kila kitu kitakwenda vizuri huku akiwatolea mfano wachezaji maarufu wa Yanga, Simba na timu nyingine ambao wamewahi kufika na kupata tiba hiyo ya kuosha nyota.
“Hata watu wa kawaida na maofisa wanafika hapa kwa ajili ya kupata huduma hii, ondoeni hofu na mambo yatakwenda vziuri,” anasema mganga huyo kijana.
Suala la makubaliano ya bei linafanyika na anakubali kupunguza bei ingawa wahusika ni watu wanaoishi ‘Ulaya’. Na kwa nafasi hiyo, meneja anaomba kupiga picha za kumbukumbu ambazo ataenda nazo Ulaya kwa kuwa kule ni mambo tofauti na huenda itamsaidia ‘fundi’ kupata wateja zaidi kutoka ughaibuni. Anapewa ruhusa.
Kazi inaanza, mchezaji anakalishwa kwenye kigoda (lazima akae kwenye kiti juu, ili nyota yake ipande), anafunikwa shuka lenye rangi nyeupe). Kazi inaanza.
Mganga huyo au fundi anachukua vitu kama ukindu anavifunga na kufunga kwenye miguu ya mchezaji ambaye amevaa jezi ya Liverpool, butka nyeupe na viatu Adidas rangi ya njano. Anachukuliwa kuku mweupe na mweusi anaachwa pale chini.
Yule kuku mweupe, huku ubani umefukizwa kwenye chetezo kikubwa kama bakuli, moshi unaanza kufuka. Mchezaji anamchukua kuku huyo na kumuweke kwenye moshi unaofuka, ghafla kuku analala kama mlevi aliyezidiwa kinywaji na anafanya hivyo huku akitakiwa kunuwia anataka apate nini, anafanya hivyo.
Wakati huo, mganga anaendelea kuandika majina ya viongozi wa timu ya mchezaji huyo ambao wanatakiwa kumsahau yule mchezaji mwingine na kumfikiria mchezaji aliyeletwa na meneja.
Baada ya hapo, karatasi lenye majina anakabidhiwa mchezaji huyo mkononi. Halafu analiweka juu ya moshi unaofuka kupitia chetezo, na mganga anachukua dawa aina mbili pamoja na mafuta fulani hiyo, anamwaga juu ya karatasi na ghafla moto unalipuka.
Meneja jasho linamtoka na mchezaji halikadhalika anaonyesha kuwa na hofu kuu. Lakini mganga anaendelea na kazi yake kwa ustadi mkubwa huku akisisitiza wakati huo ndiyo mwanzo kabisa kazi inaanza kwani kuna mengi kama kumlisha kitu kuku na kumchinja, pia kwenda makaburini kuchimbia vitu kwenye makaburi.
HALI hiyo inatisha, hiyo ni sehemu kati ya mambo ambayo hufanyika kwenye mchezo wa soka na wahusika wanasisitiza si kwa ajili ya kumdhuru mtu badala yake ni kusaidia au kumlinda mtu. Usikosea CHAMPIONI JUMATATU kujua mwendelezo wa mambo yatakavyokuwa kwa mchezaji huyo na meneja pia.

No comments:

Post a Comment