aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Friday, February 28, 2014

FAHAMU: KINACHOTOKEA BABA & MAMA WANAPOACHANA



“Nilikuwa nyumbani pamoja na Mama siku ambayo Baba alituacha. Nilikuwa na umri wa miaka sita tu, kwa hiyo sikuelewa kilichokuwa kikiendelea. Nilikuwa nimeketi kwenye sakafu nikitazama televisheni. Mama alikuwa akilia na kumsihi Baba asiondoke. Baba alishuka ngazi akiwa na sanduku, akapiga magoti nilipokuwa, akanibusu, na kusema, ‘Baba anakupenda sikuzote.’ Kisha akaondoka. Sikumwona tena kwa muda mrefu. Tangu wakati huo, nimekuwa na wasiwasi kwamba Mama ataniacha pia.”— Magreth

WAZAZI wako wanapotalikiana, huenda ikaonekana kwako kama mwisho wa ulimwengu, msiba mkubwa unaofuatwa na maisha ya taabu isiyo na mwisho. Mara nyingi mtu hulemewa na hisia kama vile aibu, hasira, wasiwasi, hofu ya kuachwa, hatia, kushuka moyo, na hasara kubwa—hata tamaa ya kulipa kisasi.



Kwa Nini Wazazi Huachana?
 
Mara nyingi, watoto hushangaa wazazi wao wanapoachana kwa sababu wazazi huwaficha matatizo yao. “Sikuamini macho yangu,” asema Rachel, aliyekuwa na umri wa miaka 15 wazazi wake walipotalikiana. “Sikuzote nilidhani wanapendana.” Hata wazazi wanapogombana mara kwa mara, huenda bado ikawa hali yenye kushangaza na kuhuzunisha wanapoachana!
  • Katika visa vingi, wazazi huachana kwa sababu mmoja wa wazazi amejihusisha katika mwenendo mpotovu kingono.
  • Katika hali nyingine, “ghadhabu na kupiga kelele na matukano” yametokeza jeuri, na kumfanya mzazi mmoja ahofie usalama wake na wa watoto wake.
 
Ni kweli kwamba ndoa nyingi huvunjika pasipo misingi halali. Badala ya kutatua matatizo, watu fulani huonyesha ubinafsi kwa kutafuta talaka eti kwa sababu “hawana furaha” au “hawapendani tena.” Vyovyote vile, kwa kuwa tu wazazi wako wameamua kutosema lolote au kutokupa majibu yaliyo wazi kuhusu talaka haimaanishi kwamba hawakupendi. Wakiwa wamelemewa na uchungu wao wenyewe, huenda wazazi wako wakaona vigumu kuongea juu ya talaka. Huenda pia wakaona aibu kukubali udhaifu wao.
 
Unaloweza Kufanya
  • Tambua kinachokutia wasiwasi. Kwa kuwa talaka hubadili karibu kila kitu maishani mwako, huenda ukajikuta ukiwa na wasiwasi kuhusu mambo ambayo mwanzoni uliyapuuza. Hata hivyo, unaweza kupunguza wasiwasi wako kwa kutambua ni nini hasa kinachokutia wasiwasi. Je ni moja ya mambo yafuatayo? 
                                    Mzazi aliyebaki ataniacha pia.
                                     Familia yetu haitakuwa na pesa za kutosha za kujiruzuku.
                                     Nimechangia talaka hiyo kwa njia fulani.
                                     Nikifunga ndoa, ndoa yangu pia itavunjika.
                                     Mambo mengine ․․․․․...............................
  • Zungumza kuhusu mahangaiko yako. Jaribu kutafuta wakati unaofaa wa kuzungumza pamoja na wazazi wako kuhusu mambo yanayokuhangaisha. Waambie jinsi ulivyo na huzuni na ulivyovurugika. Huenda watakuambia kinachoendelea na kukupunguzia mahangaiko yako. Ikiwa wazazi wako hawataki au hawawezi kukutegemeza kwa sasa, unaweza kuzungumza na rafiki mkomavu. Chukua hatua ya kwanza ili kuzungumza na rafiki huyo. Kuwa na mtu anayeweza kukusikiliza kwaweza kukufariji kwelikweli.
 
Mambo ya Kuepuka
  • Usiwe na kinyongo. “Wazazi wangu walikuwa na ubinafsi,” asema Zainab, aliyenukuliwa awali. “Hawakutufikiria wala kufikiria hatua waliyochukua ingekuwa na matokeo gani kwetu.” Inaeleweka ni kwa nini Zainab angehisi hivyo, na huenda ni kweli. Hata hivyo, ungejibuje maswali yafuatayo?  Ni madhara gani yanayoweza kutokea ikiwa Zainab angeamua kuweka kinyongo na kukasirika daima? Ijapokuwa si rahisi, kwa nini ingefaa Zainab ajaribu kuwasamehe wazazi wake kwa sababu ya uchungu ambao wamemsababishia? ․․․․․
  • Epuka mazoea yanayoweza kukudhuru. “Sikuwa na furaha, nami nilikuwa nimeshuka moyo wazazi wangu walipotalikiana,” akumbuka Zainab. “Nilianza kupata matatizo shuleni nami nikaanguka mwaka mmoja. Kisha . . . nikawa mtukutu darasani na kuanza kupigana-pigana.” Unafikiri Zainab alikuwa akijaribu kutimiza nini kwa kuwa mtukutu darasani? ․․․․․Ni kwa nini alianza kupigana-pigana? ․․․․․
Je unataka kuwaadhibu wazazi wako kwa kuwa na mwenendo usiofaa? itakusaidia nini? 
 
 
Mambo Unayoweza Kutazamia Wakati Ujao
 
Jeraha halisi, kama vile kuvunjika kwa mfupa, laweza kuchukua majuma au hata miezi kabla ya kupona kabisa. Vivyo hivyo, majeraha ya kihisia yanaweza kuchukua muda mrefu kabla ya kupona. Wataalamu fulani wanahisi kwamba majeraha mabaya ya talaka yanaweza kupona kwa miaka mitatu. Huenda huo ukaonekana kuwa muda mrefu, lakini kumbuka, lazima mengi yatendeke kabla hujarudia hali yako ya kawaida.
Kwanza, mazoea ya kawaida nyumbani ambayo yamevurugwa na talaka lazima yapangwe upya. Pia itachukua muda kabla wazazi wako hawajapata usawaziko kihisia. Kisha, ndipo wanapoweza kukutegemeza wewe ifaavyo. Hata hivyo, kadiri mambo yanavyorudia hali ya kawaida, ndivyo utakavyoanza kutulia tena.

No comments:

Post a Comment