aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Wednesday, December 11, 2013

MAZISHI YA MANDELA..ULINZI FUNGA KAZI.


Nelson Rolihlahla Mandela.
Stori:  Mwandishi Wetu na vyanzo vya kimataifa
JINSI vikosi vya ulinzi na usalama nchini Afrika Kusini vinavyopiga jeramba kujiandaa na tukio kubwa duniani la mazishi ya shujaa wa vizazi vyote, Nelson Rolihlahla Mandela, ni tisa, 10 inakamilishwa na mataifa ya Marekani, Uingereza, Urusi na kadhalika.
Nyumbani kwa marehemu Mandela Kiiji cha Qunu.
Tayari wataalamu wa mambo ya takwimu wameshatoa maoni yao kwamba Kiiji cha Qunu ambacho ndicho Mandela ‘Madiba’ atazikwa, kinaweza kuingia kwenye kitabu cha rekodi za dunia (Guinness) kwa sababu kitalindwa, kitatazamwa na kufuatiliwa kwa ukaribu na watu wengi duniani kuliko ilivyowahi kutokea.
Weka pembeni rekodi zote, kikubwa ambacho kinatisha zaidi ni jinsi Serikali za Marekani, Uingereza, Urusi, China na nyinginezo zilivyojiandaa kudumisha ulinzi katika kijiji hicho na taifa zima ili kuhakikisha viongozi wao hawapati madhara yoyote pindi wakiwa nchini humo kwa mazishi.
Vilevile upo ulinzi wa Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani, Papa Francis I, utakaoratibiwa na Vatican kuhakikisha mtumishi huyo wa kiroho hapatwi na ‘kashkashi’ zozote pindi atakapokuwa Afrika Kusini hususan Kijiji cha Qunu kumzika Madiba.
FUNGA KAZI YA ULINZI
Jeshi la Afrika Kusini ndilo linaloongoza kwa ubora barani Afrika, limeshatoa ahadi kwamba litaweka ulinzi wa asilimia 100 kuhakikisha taifa lote linalindwa na Kijiji cha Qunu kinakuwa salama.
Mkuu wa Majeshi wa Afrika Kusini, Jenerali Solly Shoke, alitoa taarifa rasmi Jumatatu iliyopita akisema: “Tunajua tupo kwenye changamoto ya ulinzi, Jeshi la Afrika Kusini linatoa uhakika kuwa litatoa ulinzi wa asilimia 100.”
Katika taarifa yake hiyo, Jenerali Shoke alisema: “Kama taifa tunajua ugeni mkubwa ambao unakuja kwenye mazishi ya Madiba, nitoe uhakika kwa kila raia wa nchi hii na wageni wetu kwamba tunaweza kulinda kila kitu bila kutegemea msaada wowote.”
Kuhusu ulinzi kutoka mataifa mengine, Jenerali Shoke alisema: “Tutashirikiana nao, vipo vikosi vya mataifa mengine vimeshaweka kambi hapa, tunashirikiana lakini hata bila wao ulinzi wetu ni wa uhakika sana.”
Waziri wa Ulinzi wa Afrika Kusini, Nosiviwe Mapisa-Nqakula alisema kwamba vikosi vyote vya ulinzi na usalama nchini humo, vinaelekeza nguvu kubwa kwenye msiba wa Mandela ili kuwalinda wageni wanaoingia na watakaoingia, vilevile raia halisi wa taifa hilo.
“Taifa lipo msibani lakini hatulii tukajisahau katika kulinda mipaka ya nchi yetu, hatujisahau kulinda uhalifu wa aina yoyote, wapo watu wetu ambao wanaweza kusababisha machafuko ya ndani kama watabaini tumejisahau ulinzi,” alisema Mapisa-Nqakula.
MAREKANI KAMA KAWAIDA YAO
Sera ya Marekani juu ya ulinzi wa rais wao inajukana kwamba popote anapokwenda lazima awe na vikosi vya majeshi ya anga, ardhini, majini, vifaa vya kivita pamoja na utitiri wa wapelelezi ambao jukumu lao ni kuhakikisha kiongozi wao haguswi na baya lolote.
Taarifa ya Ikulu ya Marekani, White House imeweka wazi kusudio lake la kuongeza ulinzi katika msafara wa Rais Barack Obama kwa sababu ya ongezeko la marais wastaafu wa nchi hiyo ambao wataongozana kwenda Afrika Kusini kwenye mazishi ya Madiba ‘Tata’.
George Bush sr. (Rais wa 41), Bill Clinton (42), George Bush jr. (43), wanatarajiwa kwenda Afrika Kusini kwenye mazishi hayo ya Madiba.
Viongozi hao wataweka historia ya aina yake duniani kwa kupanda pamoja kwenye Ndege ya Air Force One ambayo hutumiwa na rais wa taifa hilo kubwa ulimwenguni.
White House ilitoa taarifa wiki iliyopita, siku moja baada ya kifo cha Mandela kwamba marais wote wa nchi hiyo ambao bado wapo hai, watahudhuria mazishi hayo.
Katika ahadi hiyo, kiongozi aliyepata kuwa rais wa Marekani ambaye inaonekana pengine hataweza kuhudhuria ni Jimmy Carter kutokana na umri wake kuwa mkubwa hivi sasa.
Carter ni Rais wa 39 wa taifa hilo na mrithi wake, Ronald Reagan (Rais wa 40), yeye alishatangulia mbele za haki.
Kauli ya White House ina maana kuwa Makao Makuu ya Ulinzi ya Marekani, Pentagon, itatumia nguvu kubwa kuhakikisha usalama wa Obama na watangulizi wake wanakuwa salama ndani na nje ya Afrika Kusini katika kipindi chote cha msiba huo.
Kwa kawaida ulinzi wa rais wa Marekani nje ya mipaka ya taifa hilo, huongozwa na vikosi vya makachero wa CIA ambayo idadi yake huwa ni siri, makomandoo wa FBI, ndege za kivita, magari ya kivita, meli kubwa ya kivita na manowari ambayo inasadikiwa kwamba ndipo kiongozi wa nchi hiyo hulala.
KUFURU YA URUSI, UINGEREZA
Rais wa Urusi, Vladmir Putin anafanya ulinzi kwenye msiba huo uongezeke, kwani nchi hiyo nayo ina sera zake za kumlinda kiongozi wake anapokuwa kwenye ziara zake ndani na nje.
Japo si kama Marekani lakini ukweli ni kwamba Urusi nayo hutoa ulinzi wa kutosha kwa kiongozi wao kitu ambacho kinatoa ishara kuwa Afrika Kusini ni mshikemshike kadiri siku zinavyokaribia kufikia mazishi ya kiongozi huyo.
Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron, ana ulinzi wa kufuru japo ni pungufu kidogo ya ule wa Rais wa Marekani. Ulinzi wa Cameron tayari umeshaanza kutua Afrika Kusini kwa mafungu.
CHINA NA KUFURU YA KIHISTORIA
Uthibitisho wa Rais wa China, Xi Jinping, kwamba atahudhuria mazishi hayo unaongeza ‘utaiti’ wa ulinzi.
Tathmini ya awali iliyofanywa na Taasisi ya Takwimu Afrika Kusini, inaonesha kwamba jumla ya vikosi vya kigeni vya ulinzi na usalama vinaweza kufikia watu 2,500,000 mpaka siku moja kabla ya mazishi.
Taasisi hiyo imebainisha kwamba wageni watakaohudhuria nchini humo, wanaweza kufikia 21,300,000 kama hakutakuwa na udhibiti wa idadi za watu.
Habari zaidi zinasema kuwa upo ushindani wa kukodi majengo marefu nchini Afrika Kusini baina ya mataifa makubwa kama Marekani, Uingereza, China na Urusi ili kufunga vifaa vya doria na usalama.
MAMLAKA YA ANGA KUDHIBITI URUSHWAJI WA NDEGE NA HELIKOPTA
Habari zinasema kuwa katika kudumisha ulinzi na usalama, kutakuwa na urukaji wa ndege na helikopta za kivita kutoka Jeshi la Afrika Kusini na mataifa mengine hususan Marekani.
Kwa muktadha huo, Mamlaka ya Anga ya Afrika Kusini, imeeleza kuwa wanaweka mpango maalum wa urushaji wa ndege na helikopta ili kuepusha kile ambacho wamekiita ni “machafuko ya anga.”
KWA HAKIKA ATAZIKWA KWA HESHIMA KUBWA
Madiba atazikwa Jumapili hii, Desemba 15, mwaka huu kijijini kwake, Qunu, Jimbo la Eastern Cape, Afrika Kusini.
Alifariki dunia Desemba 5, mwaka huu nyumbani kwake, Johannesburg, Afrika Kusini baada ya mapafu yake kushindwa kufanya kazi.
Jinsi ulinzi huo unavyoandaliwa, mwitikio wa kimataifa ulivyo ni dhahiri kwamba atazikwa kwa heshima kubwa kuliko ilivyowahi kutokea kwa kiongozi yeyote yule duniani.
Kile kinachotokea kwa Mandela ni matunda ya msimamo wake wa kupigania haki, kupambana mstari wa mbele kuondosha mfumo wa utawala wa ubaguzi wa rangi nchini mwake, kukubali kufungwa miaka 27 jela na hatimaye kufanikiwa kuifanya Afrika Kusini kuwa taifa huru, lenye usawa pasipo kubaguana.
MUNGU AILAZE ROHO YA MADIBA MAHALI PEMA PEPONI.
SOURCE:GPL

No comments:

Post a Comment