aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Tuesday, August 6, 2013

WANAMUZIKI 10 MABILIONEA AFRIKA...

MUZIKI ni kazi, mataifa mengi, hususan katika mabara ya Ulaya na Amerika Kaskazini, umewatajirisha vijana wengi.
Angalau sasa, hata Afrika wanapatikana watu ambao wanaitwa mabilionea kutokana na kazi yao ya muziki. Hata hivyo, kwetu Tanzania mambo bado majanga, maana orodha ya wanamuziki 10 barani humu, hakuna Mtanzania anayetambulika.
Kwa mujibu wa mtandao wa Answers Africa, mwaka huu, Nigeria inaongoza kwa sababu wanamuziki wake ndiyo wametengeneza idadi kubwa ya matajiri katika orodha hiyo. Wakati Joseph Mayanja ‘Jose Chameleone’ ndiye pekee aliyechomoza kwa Afrika Mashariki.
YOUSSOU N’DOUR
Oktoba mwaka huu, atatimiza umri wa miaka 54. Ndiye mwanamuziki maarufu zaidi nchini Senegal, vilevile akitajwa kwamba ni msanii wa Afrika anayeheshimika mno kwenye mabara mengine. Mwanzoni mwa mwaka 2012 aliingia kwenye kinyang’anyiro cha urais akishindana na Rais wa zamani wa nchi hiyo, Abdoulaye Wade lakini aliondolewa kwa sababu ya utata wa saini za wadhamini wake. Aprili mwaka jana, aliteuliwa kuwa Waziri wa Utalii na Utamaduni wa nchi hiyo. Muziki wake umemuwezesha kumiliki taasisi kubwa zaidi ya habari Senegal, inayomiliki vituo vya redio na televisheni, vilevile amewekeza vitega uchumi vingi. Anatajwa kuongoza Afrika.

D’BANJ
Jina kamili ni Dapo Daniel Oyebanjo, vilevile wengi humwita Koko Master. Amezaliwa mwaka 1980. Wimbo wake wa Oliver Twist, uliotoka mwaka jana, ulimuwezesha kutamba zaidi duniani, akishika chati mpaka katika mataifa mbalimbali Ulaya. Iliingia 10 Bora katika chati ya UK Singles, ikashika namba 2 katika chati ya UK R&B.
Yupo kwenye lebo ya GOOD Music ya mwana Hip Hop wa Marekani, Kanye West. D’Banj anamiliki klabu kadhaa nchini Nigeria ambazo zipo katika mtiririko wa majina ya Koko Lounges. Anamiliki kampuni yake ya maji ya kunywa inayoitwa Koko Water. Mwaka jana, alilipwa dola milioni 1 (shilingi bilioni 1.6) na kituo kimoja cha TV wakati anaonesha shoo yake ya Koko Mansion. Ana nyumba jijini Atlanta, Marekani yenye thamani ya dola milioni 1.5 (shilingi bilioni 2.4), vilevile hulipwa dola 100,000 (shilingi milioni 160) kwa shoo.
KOFFI OLOMIDE
Jina lake kamili ni Antoine Christphe Agbepa Mumba. Analipwa dola 100,000 (shilingi milioni 160) kwa shoo. Utajiri wake japo haujafafanuliwa lakini anatajwa kama bilionea kupitia mauzo ya kazi zake na malipo ya shoo.
P-SQUARE
Wanashika nafasi ya pili. Hawa ni wanamuziki ndugu, wakiwa na majina ya Peter na Paul Okoye, raia wa Nigeria. Desemba 2011, walijiunga na lebo ya Konvict Muzik, inayomilikiwa na mwanamuziki maarufu wa Marekani, Akon ambaye asili yake ni Afrika, nchini Senegal. Wana mkataba na Kampuni ya Universal South Africa kwa ajili ya usambazaji wa kazi zao.Wanalipwa dola 150,000 (shilingi milioni 240) kwa shoo. Wana mjengo wenye thamani ya dola milioni 3 (shilingi bilioni 4.8) ambao upo kweye Mji wa Ikeja, Lagos, Nigeria. Vilevile wana mkataba wa miaka mitatu na kampuni ya simu ya Globalcom ambayo inawalipa dola milioni 1 (shilingi bilioni 1.6) kwa mwaka.

FALLY IPUPA
Sifa kubwa ambayo inambeba Fally ni kuuvusha muziki wa Kikongo kuwa wa kisasa zaidi. Anafanya shoo nyingi sana na kuingiza maelfu ya dola. Vilevile ni mwanamitindo, kwani makampuni ya mavazi jijini Paris, Ufaransa, humtumia kwa ajili ya kutangaza mavazi yake, hivyo kumlipa fedha nyingi.
2 FACE IDIBIA
Jina lake kamili ni Innocent Ujah Idibia. Ameshashinda tuzo takriban 40. Wimbo wake wa African Queen ndiyo ulimfungulia njia na mpaka sasa anaendelea kutengeneza fedha kupitia kazi yake ya muziki. Amefanya uwekezaji mkubwa nchini mwake, akimiliki klabu za usiku ambazo zinamlipa sana. Anaingiza dola 80,000 (shilingi milioni 128) kwa shoo.
HUGH MASEKELA
Huyu ni mtaalam wa muziki wa Jazz nchini Afrika Kusini. Utajiri wake unatokana na mauzo ya albamu zake pamoja na shoo. Ndiye mwanamuziki wa Afrika anayeongoza kwa kualikwa kutumbuiza kwenye matamasha makubwa duniani, hususan yale ya barani Ulaya. Anamiliki studio ya muziki iliyopo nchini Botswana.
SALIF KEITA
Ni mwanamuziki ambaye ana asili ya mwasisi wa Himaya ya Mali, Sundiata Keita.  Anamiliki kisiwa kidogo nchini Ufaransa, vilevile amewekeza maeneo mbalimbali nchini humo. Pamoja na utajiri wake, Salif anatajwa kama mtu mpole na mkarimu siku zote.

JOSE CHAMELEON
Pamoja na muziki wake, anaendesha biashara mbalimbali zinazomuingiza fedha nyingi. Anamiliki kampuni ambayo inauza simu za mkononi zenye jina lake. Ana magari ya kifahari yenye thamani kubwa ikiwemo Range Rover Sport, Cadillac Escalade na Mercedes Benz Ml 200. Ana jumba la kifahari, eneo la Seguka, Kampala. Hata hivyo, Uganda kwenyewe watu wamegawanyika, wengine wamempongeza, wapo waliopinga kwamba hana utajiri huo, huku wakimwita mwanamuziki huyo kwamba ni mfuasi wa Jamii ya Siri ‘Dini ya Shetani’ ya Illuminati.

No comments:

Post a Comment