aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Saturday, August 31, 2013

IGP aibiwa upanga wa dhahabu

Inspekta Jenerali wa Jeshi la Polisi Said Mwema 
Jeshi la Polisi limeingia katika kashfa nzito baada ya mkuu wake, Inspekta Jenerali Said Mwema, kuibiwa upanga wa dhahabu ambao ni mali ya Shirikisho la Wakuu wa Majeshi ya Polisi wa nchi za Kusini mwa Afrika (SARPCCO).
Upanga huo wenye uzito wa takriban kilo tatu na wenye thamani ya zaidi ya fedha za Tanzania Sh600 milioni, ni kielelezo kwa nchi inayokabidhiwa uongozi wa SARPCCO.
Mwaka jana Tanzania ilikuwa mwenyekiti wa SARPCCO, ambapo upanga huo ulikabidhiwa kwa IGP Mwema na Jenerali Magwashi Victoria ‘Riah’ Phiyega, ambaye ni Kamishna wa Taifa wa Polisi wa Afrika Kusini aliyekuwa amemaliza muda wake kwa wakati huo.
Hilo ni tukio la pili la wizi la mali zinazohusu ofisi ya IGP, ambapo mwaka jana ndani ya ofisi hiyo kuliibwa kompyuta ndogo (laptop), ikiwa na taarifa muhimu za kipolisi. Hadi sasa hakuna taarifa za kupatikana kwa kompyuta hiyo.
IGP Mwema alikabidhiwa upanga huo Septemba 5, 2012, katika mkutano saba wa SARPCCO uliofanyika Zanzibar na kuhudhuriwa na wakuu wa majeshi ya Polisi kutoka nchi 13, pamoja na mashirika ya kimataifa.
Upanga huo ambao unakwenda sambamba na bendera ya SARPCCO, ni moja ya vielelezo vya nchi iliyochaguliwa kuwa Mwenyekiti wa shirikisho hilo, ambaye moja kwa moja anakuwa ni Mkuu wa Jeshi la Polisi katika nchi husika.
Kwa mujibu wa taratibu za SARPCCO, vielelezo hivyo hutakiwa kuwekwa ofisini kwa kiongozi husika, ikiwa ni alama ya kila mgeni atakayeingia ofisini hapo kutambua uwepo wa wadhifa huo wa kimataifa.
Uchunguzi wa gazeti hili ulibaini kuwa IGP aligundua kutoweka kwa upanga huo wiki iliyopita, wakati akijiandaa kwenda kuukabidhi kwa mwenyekiti mpya wa SARPCCO, ambaye ni IGP wa Namibia.
Taarifa za ndani ya jeshi hilo zilibaini kuwa, IGP alilazimika kuondoka bila upanga huo alipokwenda Namibia wiki iliyopita kuhudhuria mkutano wa nane wa SARPCCO, uliofanyika Jumapili iliyopita mjini Windhoek.
Kwa mujibu wa uchunguzi, IGP Mwema alikabidhi upanga unaofanana na huo ambao siyo wa dhahabu, alioazimwa kutoka kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi la Namibia, Inspekta Jenerali, Luteni Jenerali Sebastian Ndeitunga, na kukabidhiwa kama ishara ya kukabidhiwa uenyekiti wa SARPCCO kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Uchunguzi ulibaini kuwa IGP Mwema alitoa ahadi ya kurejesha upanga halisi ndani ya kipindi cha mwezi mmoja, au Serikali ya Tanzania italazimika kutengeneza mwingine kulipa uliopotea.
Uchunguzi wa gazeti hili unaonyesha kuwa kashfa hiyo ametupiwa Mkuu wa Polisi Zanzibar, Kamishna Mussa Ali Mussa pamoja na dereva wake, ikidaiwa kuwa upanga huo baada ya kupokewa na IGP Mwema, Septemba mwaka jana uliwekwa kwenye gari la kamishna huyo.
SOURCE:MWANANCHI

No comments:

Post a Comment