aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Friday, August 23, 2013

WATANZANIA WATATU WAUAWA KWA KUPIGWA RISASI KWA TUHUMA ZA KUJIHUSISHA NA BIASHARA YA MADAWA YA KULEVYA

  Maisha Tuck Shop lililopo Barabara ya Veld, Athlone, ambapo Watanzania watatu walipigwa risasi na kufariki.
Watanzania watatu waliuawa Jumanne iliyopita jijini Cape Town, Afrika ya Kusini kwa tuhuma za kujihusisha na biashara ya madawa ya kulevya. Watanzania hao walipigwa risasi na kundi la watu waliokuwa wameficha nyuso zao nje ya duka lijulikano kama Maisha Tuck Shop lililopo katika barabara ya Veld katika kitongoji cha Athlone, jijini Cape Town.

Watanzania wawili walifariki hapo hapo na mmoja alifariki baada ya kufikishwa hosipitali. Mwanamke mmoja, raia wa Afrika Kusini, alijeruhiwa vibaya katika shambulio hilo. Mmiliki wa duka hilo, Ashim Nassoro, alisema kuwa aliona kundi la watu wakiwa na bunduki za aina ya AK-47 na pistols wakipiga risasi nje ya duka lake.

Bw. Nassoro alisema amesikitika sana na shambulio tukio hilo na kudai waliouawa walikuwa marafiki zake. Alisema yeye alikuwa ndani ya nyumba, ambayo iko karibu na duka hilo pamoja na mke wake na mtoto wake wa miaka mitatu wakati milio ya risasi ilipoanza.

“Nilikuwa ndani na nilimwambia mke na mtoto wangu walale chini mpaka milio ya risasi iishe” alisema Nassoro na kuongeza “waliwapiga risasi watu waliokuwa ndani ya nyumba halafu wakaenda kwenye duka. Walikuwapiga risasi watu wawili dukani, mmoja aliyekuwa kwenye geti na mwanamke mmoja aliyekuwa kwenye nyumba.”

Nasoro aliongeza kuwa alikuwa anawajuwa Watanzania hao kwa sababu wote wanatoka Tanzania na wamekuwa wakiishi pamoja tokea walipowasili Cape Town miaka mitano iliyopita. Mtu mwingine aliyeshughudia tukio hilo alisema kuwa waliowauwa Watanzania hao walikuwa hawana wasiwasi na walirudi kwenye gari yao taratibu na kuondoka eneo la tukio.

Kufuatia tukio hilo, polisi ilimkamata Abdus Salaam Ebrahim ambaye ni kiongozi wa kikundi kinachopiga vita dhidi ya uhalifu na madawa ya kulevya nchini humo kinachojulikana kama People Against Gangsterism and Drugs (Pagad). Abdus Salaam Ebrahim amefikishwa mahakami leo kwa mashtaka ya mauaji.

Hata hivyo, mahakama imeyaondoa mashtaka hayo kwa muda kufuatia ombi la mwendesha mashtaka ili kuruhusu uchunguzi zaidi kufanyika. Wakati hakimu akiyandoa mashtaka hayo, wafuasi wa kikundi hicho cha Pagad waliokuwa wamejazana mahakamani hapo walishangilia huku wakisema “Allahu Akbar”. Majina ya Watanzania waliouawa hayakuwekwa kwenye charge sheet.

Pagad ni kikundi kilichoanziswa mwaka 1995 kupambana na uhalifu na madawa ya kulevya kwenye jiji la Cape Town baada baada ya juhudi za serikali kulegalega. Kampeni ya kikundi hiki ilianza mwaka 1996 baada kumkamata, kumpiga na kumchoma moto hadi kufa Rashaad Staggie ambaye alikuwa kiongozi wa kikundi cha uhalifu jijini Cape Town. Serikali ya Afrika Kusini ilishawahi kudai huko nyuma kuwa Pagad ni kikundi cha kigaidi baada ya kudaiwa kulipua kwa bomu hoteli ya Planet Hollywood mwaka 1998. Hata hivyo, Pagad ilipinga kuhusika kwenye shambulio hilo.

Kikundi hiki kilipotea lakini kikaja kuibuka tena kuanzia mwaka 2011 na kampeni yake ya kuchukua mitaa inayotawaliwa na uhalifu na biashara ya madawa ya kulevya. Wadadisi wa mambo wanadai kuwa kurudi tena kwa Pagad kwa gia ya kupambana na uhalifu, hasa madawa ya kulevya, itafanya hali kuwa mbaya hasa kwenye jimbo la Western Cape.

Hivi karibuni kumekuwa na ongezeko la milipuko ya mabomu kwenye sehemu zinazouza magari na pia kwenye nyumba za makazi ya watu zilizopo Athlone na maeneo mengine jijini Cape Town. Matukio haya yamekuwa yakitokea zaidi kwenye nyuma za makazi zinazotuhumiwa kutumika kufanyia biashara ya madawa ya kulevya. Kikundi cha Pagad kimekanusha kujihusisha na matukio hayo.
Source:- JF Blog



No comments:

Post a Comment