aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Wednesday, August 21, 2013

MAMBO 100 USIYOYAJUA KUHUSU CHOKOCHOKO ZA RWANDA KWA TANZANIA.....


Historia ya Rwanda ni ndefu iliyojaa misukosuko ya kisiasa, kupinduana, vita na mauaji ya wenyewe kwa wenye yaliyosababishwa na ubaguzi wa kikabila.
 

Rwanda imekuwa ikipita katika vipindi vigumu na vya hatari. Vipindi hivi hufuatana na mauaji ya raia wa nchi hiyo, sio tu kutokana na sababu za ukabila bali pia uongozi mbaya wa kisiasa.
 

Mwaka 1959, mtawala wa Kitutsi aliyekuwa akiitawala nchi hiyo na kulalamikiwa kuwa utawala wake ulikuwa ukiwaneemesha zaidi Watutsi walio wachache, uliangushwa na Wanyarwanda wa Kabila la Kihutu.
 

Mabadiliko haya yalifuatiwa na mauaji ya takriban Watutsi 150,000. Walioponea chupuchupu walikimbilia nchi mbalimbali jirani na Rwanda. 
  Ni wakati huu wazazi wa Rais wa sasa wa Rwanda, Paul Kagame walikimbilia nchi jirani, Uganda yeye akiwa na umri wa miaka miwili.


Baada ya hapo, Wahutu wakaunda Chama cha PARMEHUTU, kikiongozwa na Gregoire Kayibanda, ambaye baadaye alikuwa Rais wa Rwanda.
 

Mtu angedhani wakati huo kuwa kwa sababu uongozi wa nchi hiyo ulichukuliwa na kudhibitiwa na mtu kutoka kabila la Wahutu waliokuwa asilimia 88 ya Wanyarwanda wakati ule, (Watutsi wakiwa asilimia 11 na asilimia moja Watwa), kusingekuwa na chokochoko tena. Utawala ungekuwa wa amani, wapi?
 

Mapinduzi ya kijeshi

Kinyume na matarajio, Julai 5, 1973 Serikali hii nayo ilipinduliwa. Mapinduzi haya yalifanywa na jeshi la Wahutu wakiongozwa na Meja Jenerali Juvenal Habyarimana, ambaye naye alikuwa Mhutu.
 

Cha ajabu, licha ya tofauti hizo za kikabila, mapinduzi hayo yalifanywa na Wahutu walio wengi wakishirikiana na Watutsi wachache. Hii ilitokana na malalamiko kuwa Rais Kayibanda alikuwa akiendesha nchi kama familia yake, akipitisha uamuzi bila kushirikiana na viongozi wengine.
 

Baada ya mapinduzi hayo, kiongozi huyo mpya alibadilisha mambo mengi ikiwa ni pamoja na kusambaratisha chama kilichokuwa kikiongozwa na Kayibanda, PARMEHUTU, badala yake akaunda Chama cha National Revolutionary Movement for Development MRND.
 

Miaka takriban 17 baadaye kutokana na kile kilichoonekana kama utawala wa kikandamizaji, Watutsi waliokuwa nje ya nchi walishirikiana na Wahutu wa ndani kuanza harakati za kuiangusha Serikali ya Habyarimana.
 

Harakati hizi ndizo zilizomwingiza madarakani Rais wa sasa, Paul Kagame. Malalamiko kama yale yaliyosababisha mapinduzi dhidi ya mtangulizi wa Habyarimana yakajitokeza tena.
Mtu anayeangalia na kuchambua hali ya mambo ilivyo hivi sasa hachelewi kung’amua kuwa hali kama ile iliyozikumba tawala za tangu utawala wa kifalme wa Watutsi na tawala za Kihutu zinajitokeza tena.
 
Na hii inaifanya hali iwe tete kuliko wakati wowote. Wengi wanaamini kama yatatokea mapigano au mabadiliko katika Serikali ya Kigali pengine hali inaweza kuwa mbaya kuliko ilivyowahi kushuhudiwa.
 
Hivi sasa Wanyarwanda hasa kutoka Kabila la Kitutsi na ambao walikuwa bega kwa bega na Rais Kagame, baadhi ya wasomi na maofisa wa juu kutoka jeshi la RPF wameikimbia Rwanda na tayari kuna kampeni za chini kwa chini kutoka makabila yote mawili kuupinga utawala wa Kagame.
 
Mbaya zaidi kuna kundi kubwa la vijana waliozaliwa baada ya mauaji ya Rwanda. Hili ni kundi kubwa na mtu yeyote ambaye amekuwa akitembelea kambi za wakimbizi kwa miaka mingi anaelewa ninachoelezea hapa.
 
Mwaka 1997 nikiwa na waandishi wenzangu tulitembelea kambi za wakimbizi kutoka Rwanda. Kulikuwa na idadi kubwa ya watoto. Mmoja wetu alimuuliza mmoja wa wakimbizi kwa utani “nyinyi mpo kwenye matatizo mbona mnazaa watoto wengi hivi, hamuoni ikiwa mnajiongezea mizigo”?
 “Hawa ndio watakuja kuikomboa Rwanda,” alijibu kiongozi wa wakimbizi huku akipigiwa makofi na kundi la vijana waliokuwa pembeni kusikiliza mahojiano, katika kambi ya Mbuba wilayani.
 
Nadharia hii imekuwa ikiendelea kwa miaka mingi. Hata tulipotembelea kambi nyingine tukiandamana na Kamishna Mkuu wa Shirika la Kuhudumia wakimbizi Ulimwenguni (UNHCR), Antonio Guateres karibu waandishi wengi hawakuficha hisia zao za kushangazwa na kasi ya kuzaana katika kambi za wakimbizi.
 
Fikiria kwa utaratibu huu watoto waliozaliwa tangu mwaka 1994 ni watu wazima. Kama ni wanajeshi ni jeshi kubwa tena lenye hamasa kubwa ya kurudi katika nchi yao Rwanda katika wakati ambapo wanaona kikwazo ni Kagame na Serikali yake.
 
Hivi Kagame anajua kuwa kundi hili halibanwi na tuhuma za mauaji ya halaiki ya Rwanda ya mwaka 1994?  Hata wale wanaotafutwa sio tena kitisho dhidi ya Serikali ya Kigali sababu ni wazee sasa, wa kuogopa ni jeshi hili kubwa la vijana. 
 
Hawa Kagame anawabana na sheria gani? Isipokuwa kwamba wanajiandaa kupigana na Serikali yake kama yeye alivyofanya kuipindua Serikali ya Habyarimana akitokea Uganda?
 
Kibaya zaidi ni kuwa makundi haya katika ukanda wa Maziwa Makuu, wana mawasiliano na kwa nyakati fulani yanasaidiana.
 
Ushauri wa Rais Kikwete
Ninaamini hiki ndicho kilichomsukuma Rais Kikwete kutoa ushauri kwa marais hawa majirani zetu kuwa wasifanye kosa wazungumze na waasi. Heri kupatana nao kwa sasa kuliko baadaye wakisharidhika kuwa wamejiandaa vizuri na wakaanza mapigano rasmi.
 
Kila mwenye macho ya kuona mbali hachelewi kumshauri Kagame chonde chonde ongea na waasi hawa, badala ya kujiridhisha kuwa ni watuhumiwa wa mauaji ya halaiki, wakati wengine mauaji hayo yalitokea wakiwa na umri wa miaka sita na kurudi chini, hawa ni jeshi kubwa lenye uwezo wa muda mrefu wa kukaa msituni, ni hatari.
 
Yapo maswali kadhaa ya kujiuliza, hivi kwa nini Rais Kagame hakioni hiki tunachokiona sisi? Kwa nini hakioni hiki ambacho amekiona Rais mwenzake Kikwete?
 
Ninaamini Rais Kikwete hakukurupuka, ana vyombo vya kiintelijensia vinavyomfahamisha kinachoendelea sio tu Tanzania, lakini hata katika mapori makubwa na Misitu ya DRC.
 
Kagame anapaswa kusoma alama za nyakati, asikimbilie kusema “watuache Rwanda tumalize matatizo yetu,” kwani baada ya mauaji ya mwaka 1994 nchi hiyo ililaumu jumuia ya kimataifakuwa  haikuisaidia Rwanda kuepuka mauaji hayo.
Kama walivyosema Wahaya kuwa “ajuna akanyonyi ajuna akakyahalala” maana ukitaka kumsaidia ndege msaidie akiwa bado ana uwezo wake wa kupaa.
 
Badala yake ametoa lugha za matusi kashfa hadi kutoa vitisho dhidi ya Tanzania, ati kwa ushauri aliopewa na Rais Kikwete, kuwa azungumze na waasi wa Democratic Forces for The Liberation of Rwanda (FDLR).
 
Kikwete alitoa ushauri huo kwenye Kamisheni ya Ulinzi na Usalama ya Umoja wa Afrika wakati wa Mkutano wa wakuu wa nchi za umoja huo uliofanyika mwanzoni mwa Juni mwaka huu, mjini Addis Ababa, nchini Ethiopia.
 
Ushauri huo umegeuka mwiba na kitanzi dhidi ya uhusiano uliokuwepo kati ya Tanzania na Rwanda, ingawa wengine tunajua uhusiano huo haukuwa barabara tangu awali kwani kiongozi huyo wa Rwanda mara kwa mara amekuwa akiisimanga Tanzania hata kabla ya ushauri huo kutolewa.  

Imekuwa kama vile jirani yetu huyu amepata turufu muhimu ya kuitishia Tanzania.
 
Kinachoshuhudiwa sasa ni vita ya maneno baina ya nchi hizi mbili yaani Tanzania na Rwanda.Vita ya maneno na majibizano ya namna hii mataifa hujikuta katika vita kamili.
 
Kwa upande mwingine wengi walishangaa kwa nini Kagame aonekane kukerwa sana wakati ushauri huo haukumhusu yeye peke yake?
 
Wakati Paul Kagame akikabiliwa na kundi linaloinyemelea nchi yake la FDLR, Joseph Kabila, wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) anapambana na waasi wa sasa wa M23,  na Rais Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda akitishiwa na makundi mawili.  Allied Democratic Force (ADF) na Lord’s Resistance Army (LRA).


Hata hivyo, si Tanzania pekee ambayo imeona hatari inayoinyemelea Rwanda bali hata moja ya makanisa nchini Rwanda.
Kanisa hilo lilipeleka ujumbe hivi majuzi hadi Ikulu ya Kagame likitabiri kuwa Rwanda inakabiliwa na matatizo makubwa na kuwa inaweza tena kudidimia katika mgogoro mkubwa. Watumishi hao wa Mungu wameishia kukamatwa na kuambiwa wanataka kuvuruga amani kuleta mgororo wa kikabila.
 
Uasi zaidi
Kila kukicha wanajeshi wa Rwanda wanazidi kulikimbia jeshi lao na nchi yao, siku zilizopita walikuwa wakikimbilia Uganda siku hizi baada ya kuzidishwa ulinzi katika mpaka wa nchi hizo mbili sasa wanakimbilia Afrika Kusini, nchi ambayo inajua kwa hakika kitu gani kinaendelea nchini Rwanda. Inawapa hifadhi ya ukimbizi wa kisiasa.
 
Miongoni mwao ni aliyekuwa Mkuu wa Usalama katika Jeshi la RPF, Luteni Jenerali Faustin Kayumba Nyamwasa. Huyu alianza kutofautiana mapema na Kagame, baadaye akamsogeza mbali na nchi hiyo. Akamteua kuwa Balozi wa Rwanda nchini India.
 
Bado Kagame aliendelea kumwona ofisa huyo tishio, hivyo akamtuhumu kuwa alihusika na milipuko ya mabomu February 2010 mjini Kigali.  Wakati Kagame akiandaa utaratibu wa kumkamata habari zikavuja, ofisa huyo akatoroka kutoka India hadi Afrika Kusini anapoishi sasa.
 
Inafahamika kuwa maofisa wenye uwezo kama wa Nyamwasa wakipata ushirikiano na wanamgambo wa Kihutu walio sehemu mbalimbali nje ya Rwanda ni rahisi kuishambulia Rwanda, ndio maana inasemekana wametumwa makachero kumuua Nyamwasa kule kule Afrika Kusini lakini ‘wakachemka’ na kuishia kwenye mikono ya polisi ambapo walikiri kutumwa na Serikali ya Kigali, kumuua Nyamwasa.
 
Mwezi Juni 2010, Kiongozi wa Timu ya mpira wa miguu wa Rwanda Brigedia Jenerali Jean Bosco Kazura, alikwenda Afrika Kusini kuangalia mashindano ya kombe la dunia, lakini aliporejea Rwanda akakamatwa kwa tuhuma kuwa akiwa huko alifanya mawasiliano na Nyamwasa na kwa maana hiyo akaingizwa katika kundi la wanaotaka kuiangusha Serikali ya Kagame.
 
Jean-LĂ©onard Rugambage, mwandishi wa habari ameuawa na makachero ikisemekana kuwa alikuwa akitumiwa na Nyamwasa.

Maofisa wa Serikali ya Rwanda wanapotetea msimamo wa Rais Kagame wa kuikejeli Tanzania wanadai kilichomkasirisha bosi wao ni kushauriwa akae meza moja na wale anaowaona kama wauaji wa halaiki wa mwaka 1994, na kuwa ushauri huo ni sawa na kucheza juu ya makaburi ya Wanyarwanda waliopoteza maisha katika mauaji hayo.
 
Hata kama ingekuwa hivyo, basi angewachukia waasi wale lakini sio Tanzania kwa sababu baada ya mauaji ya Rwanda, iwe Kagame au waasi wenyewe hakuna upande wowote uliowahi kuituhumu Tanzania kuhusika kwa namna yoyote katika mauaji hayo, kwa sababu wanajua kuwa nchi hii ilikuwa ikijua kila kilichokuwa kikiendelea na kikifanywa na kila upande kabla na baada ya mauaji hayo.
 
Na hapo ndipo lilipo ‘fumbo la imani’ kwa nini Kagame amechukia sana kwa ushauri ule.
 
Sababu nyuma ya pazia
Udhaifu wa sababu ya chuki za Kagame unaashiria  kwamba kilichoikasirisha Rwanda ni uamuzi wa Tanzania kupeleka jeshi lake lishiriki kulinda amani DRC, na sio ushauri ule.
Alijua kuwa sasa mengi  yatafumuka, ambayo tayari Tanzania inayafahamu ikichanganya na yale itakayoyagundua DRC. 
Nina mifano mingi na ushahidi wa kimazingira hebu nitaje mmoja na kumalizia makala yangu.
 
Yaliyotokea 1994
Rwanda inajua, Kagame anajua, na dunia nzima inajua kuwa mauaji ya kimbali ya Rwanda yalikolezwa zaidi ya kutunguliwa ndege ya aliyekuwa Rais wa nchi hiyo wakati huo, Habyarimana.
 
Habyarimana na mwenzake wa Burundi, Syprian Ntaryamirwa walikuwa wakitoka Arusha nchini Tanzania katika mojawapo ya mikutano yenye lengo la kuangalia namna ya kugawana madaraka baina ya Serikali ya Kigali ya wakati ule na kundi la waasi siku zile RPF.
 
Kikundi hiki cha RPF kikiwa na Watutsi wengi kilikuwa kimeanzisha mapigano dhidi ya Serikali ya Habyarimana miaka miwili kabla wakipigana kutokea nchini Uganda wakitaka Serikali itoe nafasi  kwa Watutsi karibu lakini tano waliokuwa wakiishi nje ya Rwanda.
 
Licha ya Serikali ya Habyarimana kusaini makubaliano ya kuwaingiza waasi wa RPF katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa, Wahutu ambao ndio walio wengi walikuwa hawakubaliani na jambo hili.Kwa hiyo, fikiria inakuja kufahamika kuwa Watutsi wale walioanzisha mashambulizi kutokea nchini Uganda, wametungua ndege ya Rais wa kabila lao na kumuua pamoja na makamanda wa ngazi za juu wa jeshi la Rwanda la wakati ule.
 
Ndio maana baada ya kutunguliwa ndege hiyo Aprili 1994 mauaji ya kutisha yaliyodumu kwa siku mia moja yaliendelea na kugharimu maisha ya Wanyarwanda laki  nane, wengi wao wakiwa Watutsi na Wahutu wenye msimamo wa wastani.
-Imeandikwa  na  Christopher Buke   wa  gazeti  la  mwananchi.

No comments:

Post a Comment