aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Sunday, August 25, 2013

WABUNGE WASHANGAA KODI WALIYOPITISHA...


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira imepanga kukutana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka ili waweze kuzungumzia ongezeko la kodi ya asilimia 10 ya mapato ghafi ya mashirika ambayo imesababisha kupanda kwa gharama za nyumba za Serikali.

Hata hivyo kamati hiyo inashtukia kodi hiyo sasa , wakati Bunge la Bajeti ya mwaka 2013/14 wakiwamo wajumbe wa kamati walipitisha kodi ya asilimia 10 ya mapato ghafi kwa mashirika yanayozalisha kwa faida ili kuichangia Serikali.
Akizungumza katika kikao kilichoshirikisha watendaji wa NHC, Mwenyekiti wa kamati hiyo, James Lembeli alisema kuwa ongezeko hilo ni kubwa, na kwamba limesababisha kuongezeka kwa gharama za nyumba ambazo wananchi wa kawaida wanashindwa kuzinunua.
“Ongezeko hili limechangia wananchi wa hali ya chini kushindwa kumudu gharama za nyumba, jambo ambalo linakwenda kinyume na mkakati wa Serikali wa maisha ni nyumba,”alisema Lembeli.
Aliongeza, kutokana na hali hiyo, viongozi hao watakaa pamoja na kuangalia namna ambavyo wanaweza kufanya ili waweze kupunguza gharama hizo, jambo ambalo litakwenda sambamba na mkakati wa Serikali wa kujenga nyumba za gharama nafuu kwa ajili ya wananchi wasio na kipato kikubwa.
Akitolea mfano wa nyumba ambayo ilikuwa inauzwa kwa gharama ya Sh30 milioni, sasa hivi inauzwa kwa gharama ya Sh100 milioni, jambo ambalo linaonyesha wazi kuwa, wananchi wenye kipato kidogo hawawezi kununua nyumba hizo.
Alibainisha kuwa, kutokana na hali hiyo, Serikali inapaswa kukaa pamoja na watendaji wake ili kuhakikisha kuwa, kodi hiyo inaondolewa, jambo ambalo linaweza kuwasaidia wananchi hao.
Hata hivyo, kamati hiyo imeutaka uongozi wa NHC, kurudisha hati za nyumba ambazo zilichukuliwa na baadhi ya wafanyabiashara wakubwa na kujimilikisha kinyume na taratibu.
“Kuna wafanyabiashara wakubwa wamechukua nyumba wakati wa utaifishaji, lakini waliambiwa warudishe hizo nyumba wamekataa kutoa hati,jambo ambalo linakwenda kinyume,”aliongeza.
Alifafanua, kutokana na hali hiyo, kamati hiyo imewataka watendaji wa shirika hilo kuhakikisha kuwa, nyumba hizo zinarudi mikononi mwao ili ziweze kutumika kwa manufaa ya wananchi.
Hata hivyo, Mkurugenzi Mkuu wa NHC,Nehemiah Mchechu alisema kuwa, ikiwa Serikali itapunguza kodi, gharama ya nyumba inaweza kupungua, jambo ambalo linaweza kuwasaidia wananchi wa kawaida kuzinunua.
“Tunaiomba Serikali kuangalia upya kodi zilizoongezeka, kwa sababu zimechangia kupanda kwa gharama za nyumba,”alisema Mchechu.
Alisema,mkakati uliopo ni kuhakikisha kuwa, miradi iliyoanzishwa inakwisha katika kipindi kilichopangwa ili iweze kutumika kwa wananchi.
Source: Mwananchi

No comments:

Post a Comment