aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Sunday, August 25, 2013

MATAPELI WAIGUSA IKULU


MTANDAO hatari wa matapeli unaotumia mbinu mbalimbali, ikiwemo za kujipachika vyeo vya maofisa usalama wa Taifa, sasa umefanikiwa kupenya na kuanza kutumia viunga vya Ikulu iliyopo Magogoni, Jijini Dar es Salaam, kufanikisha hujuma zao. Taarifa zilizolifikia MTANZANIA Jumapili kutoka kwa watu waliokumbwa na kadhia hiyo, zimethibitisha pasipo shaka kwamba Ikulu ya Jijini Dar es Salaam sasa inataka kugeuzwa kuwa kichaka na matapeli hao, ambao pia wamejivika undugu wa kifamilia na viongozi wakubwa nchini. 
Mtandao huo, ambao unaaminika kuumiza watu mbalimbali, ukiwalenga zaidi akina mama na wanafunzi wa vyuo vikuu nchini, anayetumikia kufanikisha utapeli huo kupitia viunga vya Ikulu, ni mvulana anayejiita Baraka Tibaijuka.

Haijajulikana mara moja kama matukio yote yanayoihusisha Ikulu yanatekelezwa na Baraka au la, lakini taarifa ambazo gazeti hili limezinasa, zinaeleza kuwa, mtu huyo ambaye amekuwa akijitambulisha kama Ofisa Usalama wa Taifa, anayefanya kazi Ikulu na mtoto wa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, ndiye ambaye amekuwa akitangulizwa mbele na mtandao huo kuwaingiza Ikulu ya Magogoni watu wanaotaka kuwatapeli.

Gazeti hili tangu lilipodokezwa juu ya taarifa hizo na kuanza kuzifuatilia kwa karibu, limebaini kuwa Baraka amekuwa akiwafikisha watu mbalimbali eneo la mapokezi Ikulu kwa maelezo kuwa anakwenda kuwaunganishia kazi na kisha kuwatelekeza, huku yeye akitokomea kusikojulikana.

Kwamba watu hao, ambao wamekuwa wakiambiwa wachangie kati ya Sh 450,000-500,000 kwa ajili ya kuwawezesha kupata kazi Ikulu, wamekuwa wakiambulia vilio na simanzi na kubaini kwamba wametapeliwa pindi wanapofikishwa katika eneo hilo la Mapokezi Ikulu, huku mwenyeji wao (Baraka) akitoweka na kuwaacha hapo wasijue la kufanya.

Wakizungumza na gazeti hili, baadhi ya waliotapeliwa kwa namna hiyo, wakiwemo wanafunzi wa vyuo vya CBE, IFM, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Tumaini na baadhi ya akina mama, wamedai kuwa kwa nyakati tofauti walifikishwa Ikulu na mtandao huo wa matapeli unaomiliki magari na pikipiki.

“Alianzisha uhusiano na mtoto wa ndugu yangu ambaye anasoma Chuo cha CBE, yeye ni mtoto wa Ofisa mkubwa wa Jeshi (jina tunalo), akamwambia yeye ni ofisa usalama wa Taifa, anafanya kazi Ikulu hivyo katika mahusiano yao, akaomba apafahamu nyumbani, lakini yule ndugu yangu aliogopa kwa sababu ya baba yake.

“Alipoona hivyo, akamwambia amuunganishe na ndugu zake wengine, hivyo akamleta kwa ‘aunt’ yetu, baada ya kutuzoea akaanza kumuambia aunt awatafute wanawake wengine ambao wataweza kuchangia kwenye Mfuko wa kutunisha kampeni kwa ajili ya kugombea urais mama yake (Anna Tibaijuka) na kwamba baada ya hapo watalipwa fadhila,” alisema mmoja wa wahanga hao.

Alisema aunt yao huyo anayeishi Kimara akawakusanya akina mama wengi na kila mmoja akachangia Sh 450,000 na kwamba alipopata fedha hizo akawaambia pia kuna nafasi za kazi zimetoka Ikulu, hivyo kama kuna mtu anataka kazi atoe pesa hiyo kwa ajili ya kuwaunganishia.

“Sasa hapo tukajikusanya wengi ambao tumemaliza vyuo, wengine wa CBE, Tumaini, IMF, UDSM na yule mtoto wa ndugu yangu alikuwepo tukachanga shilingi 500,000 kila mmoja, akatuambia tuongozane hadi Ikulu kuzipeleka hizo pesa, lakini pia akatuunganishe na watu wengine huko.

“Sasa kwa sababu tulikuwa hatujawahi kufika Ikulu, tukapata wasiwasi tukajichagua watu wawili wa kuongozana naye, tukapanda gari yake aina ya Carina ambayo ilipaki Wizara ya Elimu, tukashuka hapo tukatembea kwa miguu hadi Ikulu, tulipofika getini akawasalimia wale walinzi kama anawafahamu kwa sauti ya juu na uchangamfu.”

Alisema kabla hawajaingia eneo la mapokezi akawaambia wampe simu ili aziweke kwenye bahasha pamoja na zile pesa ili wasipate usumbufu kwenye mashine za kukaguliwa.

“Tulipoingia mapokezi Ikulu, yeye akaenda kujieleza, tukaona anatunyooshea kwa mbali, hatukujua anazungumza nini, tukakaguliwa kwenye mashine tukaambiwa tukae kwenye chumba fulani cha kusubiria, wakati huo ilikuwa ni saa saba, tukakaa mpaka saa kumi tunashtuka hatumuoni, wenzetu tuliokaa nao wanaitwa wanakwenda kuwaona watu wao, sisi mwenyeji wetu hatumuoni, simu zetu kachukua.”

“Basi tukaenda kwa walinzi kuwauliza, wakatuhoji mwenyeji wetu ni nani, tukajieleza, wakasema hawamfahamu na wakaanza kutuhoji tumefikaje hapo, tulipowaelezea wakasema tumetapeliwa na watu wengi wamelizwa kwa staili hiyo, hapo basi tukaondoka zetu,” alisema mhanga huyo.

Gazeti hili lilimtafuta Prof. Tibaijuka ili kujua kama Baraka ni mtoto wake au la, alisema: “Sina mtoto anayeitwa Baraka, kama anatumia jina langu kwa kutapeli huo ni upuuzi... na waliotapeliwa wanapenda kutapeliwa, kwanini wasingenipiga simu kuniuliza mwenyewe, mimi nashangaa…kwanza hata mimi Ikulu kwenyewe nakwenda kwa appointment, tena ya shida,” alisema Prof. Tibaijuka.

MTANZANIA Jumapili liliwasiliana na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, ambaye alisema hana taarifa za kijana huyo, lakini alikiri kuwa matukio kama hayo yapo na ni ya kawaida ya kihalifu.

“Binafsi sina taarifa kama hizo, kwa kawaida matukio kama hayo tunalitaarifu Jeshi la Polisi, ambao wao ndio watachukua hatua, ni matukio ya kawaida ya kihalifu,” alisema Balozi Sefue.

Uhalifu wa utapeli unaonekana kuota mizizi hasa katika jiji la Dar es Salaam, lakini kinachotushtua ni kitendo cha matapeli hao kuanza kutumia eneo nyeti na linaloheshimika kama Ikulu ya Jijini Dar es Salaam
.

No comments:

Post a Comment