aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Saturday, August 10, 2013

HUU NDIYO UTAJIRI WA BILIONEA ALIYEUAWA

Na Mwandishi Wetu, Arusha
MAUAJI ya mfanyabiashara bilionea wa Mererani na jijini Arusha, Erasto Msuya aliyeuawa kwa kumiminiwa zaidi ya risasi 20 kwa bunduki ya Sub Machine Gun (SMG) yameibua mazito ikielezwa kuwa jamaa huyo ameacha utajiri wa kutisha.
Mwili wa Erasto Msuya (kulia) baada ya kupigwa risasi. Kushoto ni gari alilokuwa anatumia.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa Erasto ameacha vitega uchumi vingi ikielezwa kuwa ni miongoni mwa wafanyabiashara wa Mererani wanaoongoza kwa utajiri mkoani hapa, Kilimanjaro na Manyara.
Erasto ambaye aliuawa na watu wasiojulikana Jumatano iliyopita saa 7:00 mchana wilayani Hai, Kilimanjaro akitokea Mererani ni mnunuzi na mmiliki wa machimbo ya madini aina ya tanzanite hivyo alikuwa ni mtu mwenye fedha nyingi.
Hoteli ya Mezza Luna ambayo ni mali ya marehemu Erasto.
UTAJIRI
Imefahamika kuwa katika kipindi cha uhai wake, utajiri wa Erasto ulitokana na uchimbaji na biashara ya madini ya tanzanite katika mji huo mdogo.
Kutokana na biashara zake hizo, alimudu kumiliki mali nyingi zikiwemo nyumba za kifahari za kupangisha na kuishi jijini hapa, Manyara na Kilimanjaro.

ALIISHI KAMA PEPONI
Erasto ameacha jumba la kifahari alilokuwa akiishi kama yupo peponi lililopo maeneo ya Ngaramtoni jijini hapa.
Ilielezwa kuwa jamaa huyo alikuwa akimiliki maghorofa kadhaa mkoani Arusha na huko Mererani.
Kwa mfano, kwa Mererani ndiye mtu wa kwanza kumiliki ghorofa lililopo jirani na stendi kuu.

MAHOTELI
Habari zilizidi kumwagika kuwa Erasto ameacha hoteli nyingi, zikiwemo SG Resort na Mezza Luna zilizopo jijini hapa.
Ilifahamika kuwa hoteli ya SG aliijenga kwa mabilioni kutoka mfukoni mwake na si mkopo wa benki kama wanavyofanya matajiri wengine.

NDEGE BINAFSI
Kama ilivyokuwa kwa matajiri wengine waliofariki miezi kadhaa iliyopita kama Babu Sambeke na Wakili Mawalla, Erasto naye alikuwa akimiliki ndege (private jet) aliyokuwa akiitumia katika biashara zake.

MAGARI YA KIFAHARI
Pamoja na hoteli na majumba ya kifahari, marehemu huyo ameacha magari kibao ya kisasa likiwemo Range Rover Vogue New Model alilokuwa nalo wakati anauawa.
Kwa mujibu wa mmoja wa wafanyakazi wake (jina tunalo), gari hilo alilinunua hivi karibuni kwa dola za Kimarekani 250,000 (zaidi ya shilingi milioni 400 za Kitanzania).
Alisema gari hilo ni toleo la mwaka huu na aliliagiza moja kwa moja kutoka nchini Marekani.
Mbali na gari hilo, mfanyakazi huyo alieleza kuwa Erasto ameacha magari mengine ya kifahari kama Mercedes Benz, Range Rover Sport, Toyota Land Cruiser V8 na magari ya kawaida.
Pia ameacha utitiri wa magari ya kutembeza watalii kwenye mbuga mbalimbali za wanyama.

VITEGA UCHUMI
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa Erasto alikuwa akimiliki makampuni kadhaa ya utalii, nyumba za kulala wageni ‘gesti’ hasa katika Mkoa wa Manyara.
Kufuatia kifo hicho, watu waliofurika eneo la tukio walikuwa wakielezea utajiri huo huku wakizililia mali hizo kwa kuwa ameondoka na kuziacha.

MAZISHI
Habari ambazo zililifikia gazeti hili dakika za mwisho, zilieleza kuwa mazishi ya bilionea huyo yalitarajiwa kufanyika leo baada ya makubaliano ya wapi pa kuzikia kama ni Arusha au Upareni.

NINI KIMETOKEA?
Erasto aliuawa na watu wasiojulikana kati ya Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (Kia) na Mji wa Bomang’ombe katika Mtaa wa Wasomali eneo la Mjohoroni wilayani Hai, Kilimanjaro huku ikidaiwa kuwa tukio hilo lilitokana na visasi hivyo kuzua maswali mengi kuliko majibu.

No comments:

Post a Comment