aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Sunday, August 4, 2013

DK. SLAA AMKOSOA KIKWETE KUSHAURI KAGAME AZUNGUMZE NA WAASI, AHOJI MBONA YEYE HAZUNGUMZI NA WAPINZANI

CHANZO: NIPASHE
Katibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Wilbroad Slaa, amemkosoa Rais Jakaya Kikwete, kuhusu kauli ya kumshauri Rais wa Rwanda, Paul Kagame, kuzungumza na waasi wa serikali yake.

Dk. Slaa amesema haoni busara kwa Rais Kikwete kuwaambia viongozi wa Rwanda, akiwamo Rais Kagame, kuzungumza na wafuasi wa chama cha FDRL walioko Congo kwa vile wanatambulika kama wauaji.

Alisema hayo wakati akizungumza katika kongamano la vijana wa Chadema (Bavicha) la uchumi na ajira lililofanyika jana jijini Dar es Salaam.

Alimshangaa kuwataka kuzungumza na watu ambao Kagame anawaita wauaji wenye asili ya kundi la jeshi la Nterahamwe, lililokuwa linaangamiza Watutsi.

“Rais Kikwete hapa nyumbani hawezi kuzungumza na wapinzani , hajachukua hatua dhidi wauaji wa mwandishi Daudi Mwangosi, alishauriwa amuwajibishe Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa Michael Kamuhanda , amempandisha cheo,” alisema.

Alisema Rais alitakiwa kuwaambia waje awapatanishe lakini si kuwaambia wazungumze na watu anaowatuhumu kuua Watutsi.

Kumezuka sitofahamu ya uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Rwanda, baada ya Rais Kikwete kutoa ushauri huo wakati wa mkutano wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika Addis Ababa, Ethiopia hivi karibuni.

Ushauri huo ulionekana kumchukiza Rais Kagame, anayedaiwa kuhutubia mikutano kadhaa nchini kwake na kutumia lugha ya matusi, kejeli na dhihaka dhidi ya Rais Kikwete na Tanzania.

AJITOSA UFISADI GLOBAL PARTNERSHIP DIALOGUE
Dk. Slaa amejitosa katika sakata la tuhuma za ufisadi wa mabilioni ya fedha, zilizopaswa kugharamia wageni wakiwamo marais walioshiriki mkutano wa Global Partnership Dialogue jijini Dar es Salaam na kusema matumizi mabaya ya fedha za umma yanakuza tatizo la ajira.

Alidai kuwa fedha hizo zilizotumiwa kuwalipia malazi na usafiri wa ndege wageni hao hazijatolewa maelezo licha ya Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa kuahidi kulizungumzia.

Dk. Slaa alidai kuwa, matumizi ya fedha kwa mtindo huo wa kukosa uwazi hayafanyika popote ila Tanzania peke yake.

Kadhalika alidai ufisadi na matumizi mabaya ya fedha za umma yalihusisha uidhinishaji wa Shilingi trilioni 1.7 zilizotolewa wakati wa mdodoro wa uchumi kwa washirika kampuni zisizofahamika.

Dk. Slaa alidai fedha hizo zilizotolewa siku tatu kabla ya kikao cha bajeti kwa kuwazawadia washirika na kampuni ‘hewa’ zimehojiwa na Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG) lakini hakuna maelezo.

Alisema fedha za kuokoa mashirika zilitolewa India, Marekani, Ghana na Uingereza lakini kwa utararibu wa uwazi si kama ilivyotokea kwa Tanzania a

mbapo zoezi lilitawaliwa na usiri mkubwa.


KONGAMANO LA BAVICHA
Aliwataka vijana kutumia ubunifu , kutochagua kazi na kujituma ili kukabiliana na ukosefu wa ajira .

Alishauri serikali kuendeleza vipaji badala ya kugombana na wabunifu na kusumbuana na wabunifu wanapojitokeza akitoa mfano wa kugombana na wagunduzi wa bunduki za magobore.

Alieleza kuwa ukosefu wa ajira unachangiwa na ufisadi, kukosa vipaumbele na kutoa kazi kwa kujuana badala ya kuzingatia sifa.  

No comments:

Post a Comment