aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Sunday, August 11, 2013

SERIKALI IMESHINDWA KUDHIBITI MAUAJI....


Wiki inayomalizika leo, wananchi waliendelea kushuhudia matukio makubwa ya mauaji na vitendo vingine vya kihalifu vinavyoashiria kwamba Jeshi la Polisi na mamlaka nyingine za usalama pengine hazina tena uwezo au utashi wa kulinda raia na mali zao. Hali ya usalama imeendelea kuzorota kwa kasi ya ajabu, hivyo hakuna mwananchi anayeweza kujidanganya hivi sasa kwamba maisha yake yako salama na kwamba atapata mahali pa kukimbilia iwapo maisha yake yatakuwa hatarini.
Tunaelewa fika kwamba kauli hiyo hapo juu ni nzito, lakini tumeitoa bila woga wala kutafuna maneno kwa kutilia maanani ukubwa wa tatizo. Tatizo la mauaji ya watu wasiokuwa na hatia katika nchi yetu hivi sasa ni kubwa. Silaha zimezagaa ovyo mitaani na zinauzwa kama njugu, huku zikitumika kuwaua watu kwa lengo la kupora mali zao, kuwatia vilema vya maisha au kulipiza visasi. Hali hiyo ni mbali na mashambulizi wanayofanyiwa baadhi ya watu kwa lengo la kuwadhuru, ikiwa ni pamoja na kuwamwagia tindikali, kuwateka nyara, kuwanyofoa macho na kuwang’oa meno na kucha.
Hoja yetu kuu hapa ni kwamba, wananchi wamejaa woga na hofu kwa kutokuwa na uhakika wa usalama wao. Jambo linalochochea hali hiyo ni Jeshi la Polisi kutoonekana kufadhaishwa wala kukerwa na hali hiyo.Baya zaidi ni pale Serikali inapobaki tu kuwa mtazamaji wa hali hiyo ya kutisha pasipo kubuni mbinu za kuhakikisha Jeshi la Polisi linawajibika vilivyo. Inakuwaje kila kukicha mauaji yanaendelea katika sehemu mbalimbali nchini, huku Polisi nao wakithibitika kuhusika na vifo vya raia wasio na hatia katika baadhi ya matukio?
Katikati ya wiki, wafanyabiashara wawili maarufu katika Mikoa ya Arusha na Manyara waliuawa katika matukio tofauti kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana. Kama hiyo haitoshi, siku mbili zilizopita mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliuawa jijini kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana wakati akitoka benki, huku wasichana wawili raia wa Uingereza wakimwagiwa tindikali mjini Zanzibar na watu wasiojulikana. Kuhusu tukio la Zanzibar vyombo vya habari duniani kote vimeandika na kutangaza sana tukio hilo, ambalo linasemekana litaathiri sana utalii wa Zanzibar kwa muda mrefu.
Kama tulivyoeleza hapo juu, matukio hayo ni kama tone moja tu la maji katika Bahari ya Hindi, kwani matukio ya aina hiyo katika kipindi cha miezi sita iliyopita ni mengi mno kuyaorodhesha katika safu hii. Wananchi hawajasahau matukio ya kutekwa na kuteswa kwa Absalom Kibanda na Dk Ulimboka jijini Dar es Salaam, wala hawajasahau kupigwa risasi na kujeruhiwa kwa Padre Ambrose Mkenda, kuuawa kwa kupigwa risasi kwa Padre Ambrose Mushi na kumwagiwa tindikali kwa Sheikh Saroga wote wa visiwani Zanzibar.
Ajabu ni kwamba Serikali imetia pamba masikioni na tunahisi inafanya hivyo makusudi. Ukimya wa Serikali unatokana na kulikumbatia Jeshi la Polisi na kushindwa kuliwajibisha, kwani jeshi hilo limethibitika kuibeba Serikali na chama tawala dhidi ya vyama vya upinzani. Ni maoni ya wengi kwamba mpaka pale jeshi hilo litakapojivua minyororo ya utumwa wa kisiasa, likavunja ndoa na wanasiasa na kuwa jeshi lenye weledi, ndipo tutakapoona mwisho wa mauaji na uhalifu mwingine ambao umepandikiza hofu na kuchafua taswira ya nchi yetu.

No comments:

Post a Comment