aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Monday, August 12, 2013

KISHAPU YAONGOZA KWA UTAPIAMLO...



WILAYA ya Kishapu mkoani Shinyanga imetajwa kuwa inaongoza kwa tatizo la utapiamlo kwa watoto miongoni mwa wilaya 40 nchini, ambazo hivi karibuni zilifanyiwa tathmini ya hali ya chakula na lishe.Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa hivi karibuni na Ofisa Lishe wa Mkoa wa Shinyanga, Mariam Mwita, tathmini ya hali ya chakula iliyofanywa na Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC), Septemba, 2012 katika wilaya 40 nchini matokeo yalionesha wilaya ya Kishapu ilikuwa na hali mbaya zaidi.

Akitoa taarifa hiyo mkoani Shinyanga, Mwita alisema mbali ya wilaya hiyo pia wilaya ya Shinyanga ilikuwa hatarini baada ya asilimia kubwa ya watoto waliopimwa kubainika wana utapiamlo.
Alisema takwimu za upimaji huo zilionesha asilimia 43 ya watoto waliopimwa walikuwa wamedumaa, asilimia 10 walikuwa na uzito pungufu, upungufu wa damu walikuwa ni asilimia 75, uhaba wa madini chuma asilimia 48.
Asilimia tatu ya watoto walikuwa wamekonda huku asilimia 37 wakiwa na tatizo la upungufu wa vitamini A.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Wilson Nkhambaku, alielezea kushutushwa kwake na takwimu hizo na kwamba inampa uchungu hasa pale anapokumbuka kuwa wilaya hiyo ni moja ya wilaya ambazo halmashauri zake zilitajwa pia na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuwa na hesabu chafu.
Kutokana na hali hiyo mkuu huyo ameyaomba mashirika mbalimbali ya umma na ya kibinafsi ikiwemo Shirika la World Vision kuangalia uwezekano wa kuwasaidia wakazi wa wilaya hiyo ili kuwapatia chakula kitakachoweza kuwasaidia kuboresha lishe zao.
Akizungumzia hali hiyo Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Ally Rufunga, aliwaomba wajumbe wa kamati ya lishe ya mkoa iliyoundwa kwa ushirikiano wa wadau mbalimbali kuhakikisha wanafikisha elimu ya lishe bora kwa wananchi hasa walioko maeneo ya vijijini.
Mkuu huyo aliwaomba wakazi wa mkoa wa Shinyanga kuhakikisha wanazingatia ushauri wa mara kwa mara unaotolewa na wataalam wa afya na wajitahidi kutunza afya zao vizuri ikiwemo suala la kufanya mazoezi ya viungo mara kwa mara.
“Tatizo la utapiamlo linatibika, ni muhimu tukazingatia ushauri wa wataalamu wa afya, tule vyakula vyenye lishe, tufanye mazoezi angalau muda wa nusu saa kila siku, tule milo kamili hasa kwa kuzidisha ulaji wa mboga za majani na matunda,” alisema Rufunga.

No comments:

Post a Comment