aaaaa

Pages

Ads 468x60px

Friday, August 9, 2013

JUSA AFYATUKA TENA SAKATA LA RAIA WA UINGEREZA KUMWAGIWA TINDIKALI...

Mbunge wa Mjini Mkongwe-CUF Ismail Jussa
---
Taswira ya Zanzibar kama kisiwa cha amani imechafuliwa tena jana usiku pale watu wasiojulikana walipofanya kitendo cha kinyama na kishenzi cha kuwamwagia tindikali (acid) wananchi wawili wa Uingereza katika maeneo ya Shangani, jimbo la Mji Mkongwe. 
Taarifa za awali nilizozipata ni kwamba vijana hao wawili wapo Zanzibar wakiwa ni sehemu ya vijana wanaojitolea (volunteers) katika shughuli za sanaa (Arts).
Nikiwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi wa jimbo la Mji Mkongwe, mwananchi wa Zanzibar ninayeipenda nchi yangu na pia nikiwa kama binadamu ninayethamini utu wa kila mtu nalaani vikali na kwa nguvu zote uovu na uhalifu huo ambao umekiuka misingi ya ubinadamu na utu. 
Polisi na mamlaka nyengine za nchi zinapaswa kufanya uchunguzi wa kina na wa haraka wa kuwajua ni nani waliohusika na tukio hili na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria. Hili la kuchukua hatua za haraka na za dharura na kuongeza kasi ya uchunguzi ni la muhimu sana maana sasa matukio ya hujuma kwa kutumia tindikali (acid) yamekuwa ni jambo la kawaida na yanaendelea kuongezeka. 

Tukio hili la jana linakwenda moja kwa moja na kupiga moyo wa uchumi wa Zanzibar kwa maana ya sekta ya utalii. Tusipochukua hatua za haraka na za dharura na kuonekana tunajali, uchumi wa Zanzibar unaweza kuathirika kwa kiasi kikubwa na kuyumbisha utoaji wa huduma kwa wananchi, huduma ambazo zinategemea mapato yanayotokana na utalii. 
Nilipata nafasi ya kufika haraka pale walipokuwepo waathirika wa tukio hilo mara baada ya kupata taarifa na pia kuwasindikiza hadi Uwanja wa Ndege wa Zanzibar nikiwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii naMichezo, viongozi wa Jumuiya ya Wawekezaji katika Sekta ya Utalii (ZATI) na Balozi wa Heshima wa Uingereza aliyepo Zanzibar. 

Nawapa pole wasichana hao wawili na nawaombea wapone kwa haraka. Fikra, hisia na dua zetu ziko pamoja nao. Sifa ya Zanzibar kwa karne nyingi imekuwa ni kisiwa cha amani ambacho watu wake ni wastaarabu, wakarimu na wanaopenda wageni. Mjengeko wa jamii ya yetu ya Kizanzibari wenyewe umetokana na mchanganyiko wa watu kutoka sehemu mbali mbali duniani ambao walihamia Zanzibar na kupafanya ndiyo maskani yao. Kitendo kama hichi kilichotokea jana kinakwenda kinyume na misingi ya historia yetu hiyo. 


Ni mapema kusema ni nani aliyepo nyuma ya kitendo hichi lakini jambo moja la wazi ni kuwa yeyote anayehusika amekusudia kuiumiza Zanzibar na Wazanzibari. Kuuhujumu utalii ni kuuhujumu uchumi wa Zanzibar na kuyahujumu maisha ya Wazanzibari. Wakati mamlaka zinazohusika zikiendelea na uchunguzi wa tukio hili, kuwasaka waliohusika na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria, natoa wito kwa Serikali kuchukua hatua zifuatazo: 

Kuongeza doria za polisi ndani ya Mji Mkongwe ambao bado unabakia kuwa ndiyo mji mkuu wa Zanzibar na pia kituo kikuu cha harakati zote za kiuchumi ikiwemo biashara na utalii. Kuwepo kwa Polisi Jamii chini ya dhana ya Ulinzi Shirikishi kusiwe ndiyo mbadala wa Jeshi la Polisi kutekeleza wajibu wake hasa kufanya doria za kawaida. 

Kuuwekea Mji Mkongwe kamera za mitaani za kufuatilia nyenendo za watu (surveillance cameras) hasa ikizingatiwa kuwa Mji Mkongwe ndiko kwenye harakati nyingi zinazopelekea mkusanyiko wa watu wengi wakiwemo watalii na wageni wengine wanaotembelea Zanzibar. 

Mji Mkongwe kurejeshewa huduma ya taa za njiani na za mitaa (street lights) ili kuongeza usalama wa watu wakiwemo wageni wanaotembelea eneo hili ambako kuna idadi kubwa ya hoteli za kitalii. 

Jeshi la Polisi Zanzibar limekuwa likilalamika kwa kuwa na bajeti ndogo isiyokidhi mahitaji ya kutekeleza wajibu wao ipasavyo ikiwa ni pamoja na kutokuwa na usafiri wa uhakika, mafuta na vifaa vya kazi. Mamlaka zinazohusika zinapaswa kukaa pamoja na kutatua matatizo haya. 

Serikali, Jeshi la Polisi, na mamlaka nyengine zinazohusika pia wanapaswa kuwa na vikao vya mashauriano vya mara kwa mara na Jumuiya ya Wawekezaji katika Sekta ya Utalii (ZATI) na Jumuiya ya Watoa Huduma za Usafirishaji na Utembezaji Watalii (ZATO) ili kushughulikia matatizo mbali mbali yanayojitokeza hususan yale yanayohusu masuala ya usalama wa wageni wanaotembelea Zanzibar.
Mwisho, natoa wito kwa wananchi na wakaazi wote wa Mji Mkongwe na Zanzibar kwa ujumla kuwa makini na kufuatilia nyenendo zinazotia mashaka au zinazoashiria mwelekeo wa kufanya vitendo vya uhalifu ndani ya Mji wetu na ndani ya Zanzibar au hata nje ya Zanzibar na pale wanapobaini mwelekeo kama huo kutoa taarifa haraka kwa mamlaka zinazohusika. ISMAIL JUSSA MJUMBE WA BARAZA LA WAWAKILISHI JIMBO LA MJI MKONGWE a na Jumuiya ya Wawekezaji katika Sekta ya Utalii (ZATI) na Jumuiya ya Watoa Huduma za Usafirishaji na Utembezaji Watalii (ZATO) ili kushughulikia matatizo mbali mbali yanayojitokeza hususan yale yanayohusu masuala ya usalama wa wageni wanaotembelea Zanzibar. 

Mwisho, natoa wito kwa wananchi na wakaazi wote wa Mji Mkongwe na Zanzibar kwa ujumla kuwa makini na kufuatilia nyenendo zinazotia mashaka au zinazoashiria mwelekeo wa kufanya vitendo vya uhalifu ndani ya Mji wetu na ndani ya Zanzibar au hata nje ya Zanzibar na pale wanapobaini mwelekeo kama huo kutoa taarifa haraka kwa mamlaka zinazohusika. 


ISMAIL JUSSA 
MJUMBE WA BARAZA LA WAWAKILISHI 
JIMBO LA MJI MKONGWE

No comments:

Post a Comment